Idara ya mahakama katika kaunti ya Kwale imetishia kuzifunga nyumba saba za watoto zilizo katika eneo bunge la Lunga-lunga, baada ya kubainika kwamba taasisi hizo hazijasajiliwa, zina usimamizi duni na zinajihusisha na vitendo haramu ikiwemo ulanguzi wa watoto.
Akizungumza katika eneo la Tsuini,Vanga huko Lunga-lunga jaji wa mahakama kuu ya ardhi na mazingira kaunti ya Kwale Lucas Naikun amesema hakuna taasisi itakayoruhusiwa kuhifadhi watoto pasi na kukamilisha mchakato wa usajili na serikali.
Naikun aidha amesema watoto wako chini ya ulinzi wa serikali na kwamba nyumba yeyote inayohifadhi watoto pasi na kuidhinishwa kwa njia za kisheria, moja kwa moja inakua tishio kwa usalama wa watoto.
Kwa upande wake hakimu Leah Kabaria amesema mahakama imeshughulikia kesi 72 za dhulma za kingono dhidi ya watoto, akisema hali hiyo inaashiria ongezeko la dhulma dhidi ya watoto.
Kaberia amesema tayari watoto 27 wameondolewa nyumbani kwao baada ya maafisa kugundua kwamba watoto hao hawapati huduma bora, wametelekezwa au wanalazimishwa kuingia katika ndoa za mapema.
Story by Mimuh Mohamed/Mwanaamina Fakii



