ODM Yajizatiti Kuimarisha Umoja na Uthabiti Kabla ya Uchaguzi wa 2027
Chama cha ODM kinapaswa kuwa imara hata zaidi na kuendelea kujiandaa
kwa uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2027.
Seneta wa Kaunti ya Kilifi Stewart Madzayo aliye Kiongozi wa wachache
katika Bunge la Seneti amehoji kwamba kwa sasa jambo la msingi chamani ni
kujenga udhabiti wa chama na kuziba mianya ya mgawanyiko na malumbano
ili chama hicho kisiporomoke.
Kulingana na Madzayo, si kinyume kwa chama hicho kuungana na vyama
vingine vya kisiasa katika kuunda Serikali baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka
wa 2027, akiwataka wanachama na Viongozi wa chama cha ODM kumakinika
katika kukidhibiti chama.
Kauli sawa na hiyo ilitolewa hapo awali na Katibu mkuu wa chama
cha ODM Edwin Sifuna aliyehoji kwamba umoja wa chama ndiyo kipengele
kikuu atakachokitilia mkazo katika uongozi wake.
Semi hizo zinajiri huku Kaunti ya Mombasa ikijiandaa kwa shamrashamra za
kuadhimisha miaka 20, tangu kuasisiwa kwa chama hicho, sherehe
zitakazoanza Novemba 14 hadi 16 mwaka huu.