Serikali ya kitaifa imefichua kwamba imefanikiwa kuwaokoa wakenya 18 waliokua wamesajiliwa katika vita vinavyoendelea kati ya Urusi na Ukraine.
Kulingana na wizara ya masuala ya kigeni, wakenya hao wameokolewa baada ya kupiga simu wakiwa katika hali ya mfadhaiko, na tayari wamepewa nakala za dharura za kusafiri ili kurejea humu nchini.
Mkuu wa mawaziri Musalia Mudavadi kwenye taarifa yake siku ya Jumatano, amesema wakenya hao pamoja na familia zao watapewa ushauri nasaha ili kuwasaidia kisaikolojia.
Mudavadi amesema tangu kuanza vita kati ya Urusi na Ukraine, jeshi la Urusi limekua likisajili wanajeshi hadi kutoka mataifa ya Afrika na kwamba wanaripoti zinazothibitisha kwamba zaidi ya wakenya 200 wamesajiliwa katika jeshi la Urusi.
Mudavadi amesema ubalozi wa Kenya mjini Moscow umethibitisha kuna wakenya waliojeruhiwa katika vita hivyo, na wamepokea barua pepe na jumbe za dharura za wakenya waliokwama Urusi.



